..

..
.

Friday 16 November 2012

William Hague kukutana na viongozi wa muungano wa upinzani Syria

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Uingereza William Hague




Viongozi wa muungano wa upinzani nchini Syria ulioundwa hivi karibuni, leo wanatarajiwa kukutana na waziri wa mambo ya nje wa Uingereza William Hague mjini London.
Kulingana na shirika la utangazaji la BBC, Mkuu wa muungano huo wa Upinzani nchini Syria, Ahmed Moaz al-Khatib, pamoja na wanachama wengine watatu wa muungano huo wanatarajiwa kukutana na waziri wa mambo ya nje wa Uingereza William Hague. Uingereza inania ya kuutaka muungano huo kuweka wazi mpango wao juu ya kipindi cha mpito nchini Syria.
Uingereza imesema pindi tu muungano huo utakapofanya hivyo, basi itatilia maanani swala la kuwatambua rasmi kama muungano halali wa upinzani kwa utawala wa rais Bashar Al Assad. Tayari Ufaransa, Uturuki na mataifa ya eneo la Guba yanautambua rasmi muungano huo wa upinzani.
Wanachama wa muungano mpya wa upinzani, Syria Wanachama wa muungano mpya wa upinzani, Syria
Huku hayo yakiarifiwa ndani ya Syria kwenyewe, wanaharakati wa upinzani wanasema vikosi vya serikali vimeanza kulishambulia eneo linalokaliwa na waasi la al Rastan mjini Homs. Mashambulizi mengine yameripotiwa katika mji wa al-Zabadani nje kidogo ya mji mkuu Damascus. Kulingana na shirika la kutetea haki za binaadamu la Syria lililo na makao yake mjini London, takriban watu 140 wameuwawa katika mashambulizi ya jana pekee.
Kwa upande mwengine Ufaransa imesema itazungumza pamoja na wanachama wengine 27 wa Umoja wa Ulaya juu ya pendekezo la kupunguza vikwazo vya silaha vya Umoja huo ambavyo kwa sasa vinazihusu pande zote mbili zinazohusika na vita vya Syria. Lakini Urusi imesema hatua yoyote ya aina hiyo itakuwa ni kukiuka sheria ya kimataifa .
Jengo moja likiwaka moto nchini Syria Jengo moja likiwaka moto nchini Syria
Kwa Upande wake waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa Laurent Fabius amesema hatua ya waasi kupewa silaha ni njia moja ya kuwalinda kutokana na mashambulizi makali yanayofanywa na vikosi vya serikali ya Assad.
"Hakuna haja ya kuupa sura ya kijeshi mzozo huu. Lakini haikubaliki pia kuona maeneo yaliyokombolewa,yanashambuliwa kwa mabomu. Lazima pawepo wizani,na si rahisi. Kwa upande mmoja kutoingilia upande wa kijeshi na upande wa pili kuzuwia maeneo yaliyokombolewa yasibomolewe. Ndio maana suala la kupelekwa silaha za kujilinda linabidi lizushwe hapa." amesema Laurent Fabius
Umoja wa Mataifa walalamika
Wakati huo huo kwa mujibu wa barua iliyolifikia shirika laahabari la AFP hapo jana Umoja wa mataifa umelalamika kwa serikali ya Syria kwa kudai kwamba ilikuwa na ruhusa ya umoja huo kuwashambulia waasi katika eneo la milima ya Golan ambalo halipaswi kuwa na harakati zozote za kijeshi.
Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia amani Herve Ladsous Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia amani Herve Ladsous
Katika barua iliotumwa kwa balozi wa Syria, Mkuu wa Umoja huo anayeshughulika na swala la amani Herve Ladsous, aliitaka Syria kusimamisha mashambulizi hayo mara moja katika maeneo hayo ya kijeshi yalio kati ya Syria na Israel ambayo huenda yakahatarisha maisha ya raia pamoja na waangalizi wa Umoja wa Mataifa walioko huko.
Tangu kuanza kwa mapigano nchini Syria miezi 20 iliopita tariban watu 39,000 wameuwawa

No comments:

Post a Comment

KARIBU