..

..
.

Saturday 7 July 2012

NI HATUA NZURI YA UWEZEKANO WA BINADAMU KWENDA KUISHI, DALILI ZAONYESHA KUNA VIUMBE HAI

WANASAYANSI wa anga kwa muda mrefu wamekuwa wakitafuta  uwezekano wa maisha katika sayari nyingine, mbali na dunia.Kuna imani kuwa kwenye sayari hizo, huenda zikapatikana raslimali nyingi kwa urahisi kuliko duniani ambako binadamu wameishi mamilioni ya miaka  hadi sasa.
Wataalamu hao wa anga wamekuwa wakifanya hivyo kwa muda sasa na moja ya mambo muhimu wanayoangalia ni upatikanaji wa maji. Popote maji yanapopatikana, wanaamini maisha yanawezekana.Moja ya sayari ambayo wamekuwa wakiichunguza kwa miaka mingi sasa ni Mars, ambayo ni ya nne kutoka kwenye jua. Dunia ni ya tatu.

Sababu kuu za kuichagua sayari hii tofauti na zingine ni kwamba, hali ya hewa inatofautiana kidogo sana na ya dunia.
Sayari nyingine kama Mercury na Venus, zipo karibu zaidi na jua na hali ya joto iko juu kiasi kwamba hali ya maisha inaweza kuwa taabu.


Mars ambayo wanasayansi wanaipa jina la sayari nyekundu, ipo karibu na dunia, hivyo ni rahisi kufika iwapo wanasayansi watathibitisha iwapo maisha yanawezekana huko.

Wanaiita sayari nyekundu kwa sababu eneo kubwa la uso wake ni wa rangi nyekundu, tofauti na nyingine zilizomo kwenye mfumo wetu wa sayari.

Hakuna mwanasayansi  ambaye amethubutu kusafiri hadi kwenye sayari hiyo kutokana na ugumu wa kupata vyombo vya kuaminika, vinavyoweza kusafirisha watu kutoka duniani hadi Mars na kurudi salama.

Hata hivyo, hilo siyo tatizo kwa sababu wakibaini mazingira mazuri, utengenezaji wa vyombo hivyo hauwezi kuwapa taabu.

Kazi ya uchunguzi imekuwa ikifanywa kwa vyombo maalumu ambavyo havina watu lakini, vina uwezo wa kuleta mawasiliano duniani.

Pia wanatumia viona mbali katika mchakato huo  kuchunguza hali ilivyo kwenye sayari hii, ambayo kumekuwapo na hisia kwamba huenda waliwahi kuishi viumbe hai mamilioni ya miaka iliyopita lakini baadae mazingira yakabadilika na kuwa mabaya.

Uchunguzi unaonyesha kuwa, sayari hii ina mabonde mengi ambayo yanakila dalili kuwa awali yalikuwa yanatiririsha maji kama ilivyo mito hapa duniani.

Kwa muda mrefu, wanasayansi wamekuwa wakiichukulia sayari hiyo kuwa na mazingira ya jangwa yanayotokana na ukame wa muda mrefu.

Wagundua maji
Mwezi uliopita wanasayansi hao wamekuja na maelezo kwamba sayari hiyo ina kiwango kikubwa cha maji na mengi yapo mita chache kutoka uso wake.

Mmoja wa wanasayansi wanaochunguza sayari hiyo ni Profesa Jay Melosh wa Chuo Kikuu cha Purdue, nchini Marekani.

Yeye anasema uchunguzi huo umewapa imani kwamba siyo tu kwamba Mars ina maji bali kuna viumbe wadogo, mfano wa jamii ya bacteria ambao wanaendelea kuishi humo hadi leo hii.

Ni uchunguzi ambao wanaamini una matumaini tofauti na taarifa za uchunguzi uilizopita na kizuri zaidi pia ni kubaini moja ya miezi yake miwili, maji yapo kwa wingi zaidi.

Miezi inayoizunguka sayari ya Mars ni Demos na Phobos. Phobos ndio mwezi uliogundulika kuwa na kiwango kikubwa cha maji na ndio ulio karibu zaidi na sayari hiyo.

Kwa sababu hiyo, wanaamini kwamba maisha yakianza kwenye sayari ya Mars, kuna uwezekano pia wengine wakahamia kwenye mwezi huo wa Phobos.

Taarifa za uwepo wa maji kwenye sayari hii zilitolewa kwenye mkutano wa wanasayansi wanaochunguza anga za mbali, uliofanyika Austria Juni mwaka huu.

Moja ya dalili za uwepo wa maji ni vimondo ambavyo vimekuwa vikianguka kwa wingi kwenye uso wa sayari hiyo.
Mtaalamu wa Uhandisi na Mambo ya Anga, Profesa Kathleen Howell anasema picha walizopiga maeneo ambaye vimondo vimegonga uso wa Mars, zilionyesha dalili kama za mtu aliyetupa jiwe kwenye eneo lenye tope.

No comments:

Post a Comment

KARIBU