..

..
.

Tuesday 10 July 2012

KAMATI YA BUNGE YA MAMBO YA NJE,ULINZI NA USALAMA YAMALIZA ZIARA YAKE NEW YORK

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, (NUU) Mhe. Edward Lowassa( Mb) akiwa na Kaibu Balozi wa Ubalozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa. Mhe.Lowassa akiwa na wabunge wanne wamekamilisha ziara yao ya kikazi na mafunzo, ziara ambayo ilikuwa na lengo la kujionea hali ya utendaji kazi katika vituo vya Ubalozi nchi za nje, kujua mafanikio, matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo watendaji, ikiwa ni pamoja na namna ya kutafuta njia bora zaidi za kuimarisha utendaji wa kazi ili uwe wenye tija zaidi. Aidha Kamati hiyo ilipata fursa pia ya kutembelea na kukagua mali zinazomilikiwa na serikali hususani majengo.

Na Mwandishi Maalum.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama ( NUU) Mhe. Edward Lowassa (Mb), amewaasa Maafisa wa Ubalozi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, kutotetereka wala kuyumba pale inapowapasa kutoa misimamo kwa maslahi ya nchi yao.

Ametoa wasia huo wakati alipokuwa akitoa majumuisho ya ziara ya kamati yake, ziara ambayo pamoja na mambo mengine ililenga kujifunza na kujionea hali hali ya mazingira ya utendaji kazi ya maafisa wanaoiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa.

Akimnukuu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Mhe. Lowassa alikuwa na haya ya kusema.

“ Mwalimu aliwahi kutueleza huko nyuma kwamba, jambo linaloipa heshima kubwa Tanzania licha ya umaskini wake ni namna isivyotetereka katika kukisema na kukitetea kile inachokiamini hata kama kinawaudhi wakubwa. Kwa hiyo nami ninapenda kwanza, kuwapongeza kwa utendaji wenu wa kazi, lakini kubwa na la msingi msiogope kutetea misimamo ya nchi yenu licha ya umaskini wetu” akasema Mwenyekiti wa Kamati.

Akizungumza kwa niaba ya wajumbe wa Kamati hiyo inayowajumuisha Mhe.Beatrice Shelukindo,Mhe. Rachel Masishanga, Mhe. Khalifa Khalifa na Mhe. Vita Kawawa. Mhe. Edward Lowassa, licha wa kuwaasa maafia hao kutolegeza buti zao pale linapokuja suala la kusimamia na kutetea maslahi ya taifa na utaifa. Amewapongeza maafisa hao kwa namna wavyofanya kazi kwa uhodari mkubwa ikiwa ni pamoja na ushirikiano wa hali ya juu wanaouonyesha miongoni mwao.

No comments:

Post a Comment

KARIBU