..

..
.

Monday 2 July 2012

Gari la Waziri wa Habari, Mukangara lililopata ajali na kujeruhi

Hili ndilo gari ambalo alilokuwa akitumia Waziri  wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dkt. Fenella Mukangara, na kupata nalo ajali  juzi akiwa safarini kutoka Dodoma kuelekea jijini Mwanza kikazi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Antony Luta, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo majira ya saa 3:30 asubuhi katika Kata ya Nyandekwa wilayani Igunga mkoani hapo, ikihusisha gari lenye namba za usajiri STK 8780.

Luta alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa dereva wa basi la Green Star lenye namba za usajili T939 TRA ambalo lilikuwa likitokea Kahama kuelekea Dar es Salaam, alipokuwa akijaribu kulipita lori katika mlima huku gari la Waziri huyo likitokea upande wa pili.

Dereva wa Waziri aliyetambulika kwa jina la Saidi Komando, alijaribu kulikwepa basi hilo, lakini akashindwa na hivyo gari likapinduka mara tatu na kusababisha watu watatu akiwemo Waziri Fenella, kujeruhiwa.

Kamanda Luta alisema mara baada ya ajali hiyo, Waziri huyo na majeruhi wengine walikimbizwa katika hospitali ya Wilaya ya Nzega kwa matibabu na kwamba mipango ya kuwahamishia katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma zinafanywa.

Dereva wa basi la Green Star, Daniel Chawa (32), alikamatwa baadaye na polisi wilayani Igunga, baada ya kuwa amekimbia awali na hivyo atafikishwa mahakamani.

Hali ya Dkt. Mukangara inaendelea vizuri.

Akiongea na Globu ya Jamii sasa hivi yupo Dar es salaam alikorejea jana jioni na kupata matibabu zaidi katika kitengo cha mifupa cha MOI hospitali ya Muhimbili. Amesema baada ya kuchukuliwa vipimo vyote, ameonakana hana madhara mwilini zaidi ya michubuko na  majeraha mengine madogo. Anashukuru kwamba wote walikuwa wamefunga mikanda na kwamba air-bags za gari hilo zimeokoa maisha yao.

Amewashukuru sana madaktari wa Nzega na wa kitengo cha dharura cha Muhimbili ambao walimhudumia pamoja na wa hospitali ya Regency alikopatiwa vipimo vya CT-Scan. Pia anawashukuru Watanzania wote waliomuombea apate nafuu, wakiongozwa na Rais Jakaya Kikwete.

No comments:

Post a Comment

KARIBU