..

..
.

Tuesday 10 July 2012

“FURSA YENYE TIJA: TAFAKURI YA UTUMISHI WANGU KAMA NAIBU KATIBU MKUU WA UMOJA WA MATAIFA”- DR. ASHA-ROSE MIGIRO


Hakika kila chenye mwanzo hakikosi mwisho, na kila mwisho wa jambo moja huwa mwanzo wa jingine. Ingawa huenda ni mapema sana kwangu kutoa tafakuri kamili ya muhula wangu katika nafasi ya Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, hapana shaka kabisa kuwa nafasi hiyo imenipa uzoefu maridhawa. Namshukuru Katibu Mkuu BAN Ki-moon kwa  kunipa fursa hii, kuniamini na kwa ushirikiano mkubwa wakati wote wa utumishi wangu.

Kukitumikia chombo hiki cha kimataifa kwa muda wa miaka mitano na nusu mfululizo ni heshima ya pekee ambayo daima nitaienzi  kama kilele kimojawapo  cha maisha yangu ya utumishi  wa umma.  Kila siku niliyoitumia katika Umoja huo ilikuwa ni darasa la kusukuma mbele mipaka ya ujuzi na elimu.  Nimepata kufahamu mengi zaidi kuhusu Shirika lenyewe; kuhusu dunia na watu wake, lakini pia kufahamu ukomo wa uwezo wa Umoja wa Mataifa katika kushughulikia changamoto mbali mbali zinazoikabili dunia yetu.

Utumishi wangu katika Umoja wa mataifa ulikuwa fursa adhimu iliyonipa uzoefu wa pekee. Kazi hii imeujaza moyo wangu na unyenyekevu wa dhati kwani niliingia Umoja wa Mataifa wakati ambapo  dunia inachagizwa  na  madhila  makubwa makubwa yakiwemo maradhi, umaskini wa kupindukia,  kutokuwapo kwa usawa wa kijinsia,  kuongezeka kwa vitendo vya ukatili na udhalilishaji kwa wanawake na watoto;  na changamoto nyingine nyingi. Kwa muktadha huu ilikuwa fursa ya pekee kuchangia juhudi za pamoja za kuimarisha Umoja wa Mataifa katika kutekeleza majukumu yake katika kipindi cha mazingira magumu  ya kimataifa yaliyojaa changamoto za kipekee kabisa.

Daima nitaendelea kushukuru na kuthamini kwa dhati jinsi Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Serikali na Watanzania wenzangu walivyonitia moyo na kunienzi katika kipindi chote nilichokuwa Umoja wa Mataifa. Familia yangu, ndugu na marafiki walikuwa karibu nami kwa dua na kunitia nguvu wakati wote wa utumishi wangu.  Nawashukuru sana.

Hapana shaka  kazi yangu katika Umoja wa Mataifa imeniwezesha  kufahamiana kwa karibu na viongozi wengi wa kimataifa na pia  watu mbali mbali  waliopata mafanikio makubwa duniani.  Nimeweza kufahamu kwa undani thamani ya michango yao katika kujenga amani na ustawi wa dunia.

Zaidi ya yote, sitasahau hisia nilizopata kila nilipokutana na watu wanyonge waliokuwa wanahitaji msaada wa Umoja wa Mataifa.  Nitakumbuka daima tabasamu ya mwanamke mmoja niliyekutana naye katika moja ya ziara zangu barani Afrika nilipotembelea zahanati mojawapo kati ya kadhaa zinazofadhiliwa na Umoja wa Mataifa.  Mama huyo mwenye watoto sita, alikuwa amekikumbatia kitoto chake kimoja kilichokuwa nyonde nyonde; lakini alikuwa na tabasamu iliyojaa faraja na matumaini kwa kuwa alikuwa amefanikiwa kupata bure dawa za kunusuru maisha ya mwanawe.

No comments:

Post a Comment

KARIBU