..

..
.

Saturday 2 June 2012

Taifa Stars kuiduwaza Ivory Coast

                                     Wachezaji wa Taifa stars wakiwa mazoezini

TIMU ya Taifa ya Tanzania, (Taifa Stars), leo ina kibarua 'kinene' cha kusaka ushindi dhidi ya Ivory Coast watakaokuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Felix Houphouet-Boigny, jijini Abidjan katika mchezo wa kwanza kuwania kufuzu fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil mwaka 2014.Mchezo wa leo unatarajia kuanza saa 11 jioni kwa saa za Ivory Coast ikiwa ni saa mbili usiku kwa saa za Afrika mashariki.
Stars iliyowasili Abidjan juzi jioni, inatazamia kupata kibarua kikali kutoka kwa Ivory Coast iliyokusanya mastaa wake wote wakali wanaocheza soka la kulipwa barani Ulaya wakiongozwa na Didier Drogba.
Stars ambayo kocha wake, Kim Poulsen anajivunia zaidi mshambuliaji wa kimataifa anayecheza soka la kulipwa katika klabu ya TP mazembe, Mbwana Samata, jana jioni ilifanya mazoezi ya mwisho kwa ajili ya pambano hilo katika uwanja Felix Houpheut Boigny.
Ingawa hakutaka kuweka wazi, lakini kwa mujibu wa mazoezi ya jana, kocha Kim Poulsen anatazamiwa kufanya mabadiliko mawili katika kikosi chake kilichotoka suluhu na Malawi Mei 26 katika Uwanja wa Taifa.
 Bocco , Amir kuanza mechi:
Mlinzi Amir Maftaha anatarajia kuanza upande wa kushoto akichukua nafasi ya Waziri Ally ambaye katika pambano la kirafiki la kimataifa dhidi ya Malawi alionekana kuyumba kutokana na kukosa uzoefu katika mechi za kimataifa.
John Bocco, ambaye ndiye mchezaji mrefu zaidi katika kikosi cha Stars cha sasa anatazamiwa kuanza katika safu ya ushambuliaji akiziba nafasi ya Haruna Moshi ‘Boban’ ambaye alianza katika pambano dhidi Malawi lakini ameachwa nyumbani kwa kuwa majeruhi.
Hii ina maana Samata atacheza nyuma ya Bocco atakayebaki mbele peke yake, tofauti na pambano lililopita ambapo Boban alicheza nyuma ya Samatta.
Poulsen adai hana hofu:
Wakati homa ya pambano hilo ikiendelee kuwanyemelea wachezaji wa Stars ambao wamekuwa wakinyooshewa vidole vitatu na mashabiki wa Ivory Coast katika mitaa wanayopita ikiwa ni ishara ya kufungwa mabao matatu, kocha Poulsen amedai hana hofu kabisa na Ivory Coast na akawataka wachezaji wake wafanye kazi iliyowaleta na kugeuza nyumbani wakiwa mashujaa.
“Sina hofu na hata wachezaji wangu kama unavyowaona hawana hofu. Tunawaheshimu Ivory Coast wana wachezaji wenye majina makubwa kama Didier Drogba lakini nimewaambia wachezaji wangu waje kupambana na sio kucheza na majina.”
Poulsen alisema kikosi chake kitacheza kwa kadri kiwazavyo na hana mpango maalumu wa kuwadhibiti mchezaji mmoja mmoja wa Ivory Coast.
“Tutacheza kwa nidhamu katika ulinzi na tutakuwa tunaangalia namna ya kubadilika kadri mechi inavyokwenda. Lakini mpango wa kumlinda mchezaji mmoja mmoja kama Drogba au Gervinho hatuna. Tunahitaji nidhamu ya ulinzi wa pamoja,” alisema Poulsen.
Kwa upande wa Ivory Coast, kocha wao Francois Zahoui ambaye ni staa wa zamani wa timu ya taifa ya nchi hiyo aliyechukua nafasi ya kocha maarufu, Sven-Goran Eriksson alisema anaihofia Stars kwa sababu haifahamu vizuri.
“Sijawahi kuiona ikicheza kwa hiyo naihofia. Timu nyingi ndogo zimekuwa zikicheza vizuri katika miaka ya karibuni. Hatuwezi kuwadharau hata kidogo kwa sababu mpira wa siku hizi umebadilika,” alisema Zahoui.
Timu hiyo itamkosa kiungo wa Manchester City, Yaya Toure, pamoja na Emmanuel Eboue, Arthur Boka, Cheik Tiote, Souleymane Bamba, na Didier “Maestro” Zokora walioamua kupumzika kicheza timu ya taifa.
Tembo hao wanategemea kuziba nafasi hizo kwa kuwatumia chipukizi Marco Ne, Lacina Traore na Viera Diarrassouba.
Magazetini, Ivory Coast wanaonekana wameshashinda mchezo huo dhidi ya Tanzania ambayo haijawahi kufuzu kwa Kombe la Dunia hata mara moja.
Lakini mzozo wa sasa kuhusu uteteuzi wa kocha wa timu hiyo unaweza kuwa faida nyingine kwa Taifa Stars.
Mechi nyingine ya Kundi C itachezwa kaskazini mwa Afrika kwa Gambia kuikabili Morocco usiku huo.

No comments:

Post a Comment

KARIBU