..

..
.

Sunday 10 June 2012

MAMLAKA YA MAJI ARUSHA YALALAMIKIA HUJUMA



MAMLAKA ya maji safi na maji taka Jijini Arusha(AUWSA ),imebaini kuhujumiwa wa watu mbalimbali wakishirikiana na wafanyakazi wake, wasio waaminifu kwa kuunganisha maji kinyume cha utaratibu na kusababisha upotevu mkubwa wa  mapato.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa AUWSA, Eng.Ruth Koya alisema jana kuwa, tayari wamefanikiwa kuwanasa wezi wa maji zaidi ya 100 waliojiunganishia  kinyume  na utaratibu,  wakiwemo vigogo  wa halimashauri ya Arusha,ambao wamekuwa wakitumia huduma hiyo kwa kipindi kirefu,bila kulipa chochote na kuisababishia hasara kubwa mamlaka hiyo.

Vigogo wa halmashauri waliokamatwa ni pamoja na Afisa mali asili, mazingira na ardhi, Maico Myairwa ambaye yeye aling’oa  kabisa mita ya idara ya maji, ambayo imekutwa chumbani mwake, ameificha huku akijua ni kosa kisheria.

Mwingine ni fundi mkuu wa maji wa halmashauri ya Arusha,Loishono Mollel ambaye  amejiunganishia maji  baada ya kutoboa bomba kubwa la idara ya maji na kupitisha mpira mrefu kwa chini, hadi nyumbani kwake ambapo pia alikuwa akiyatumia maji hayo kustawisha  bustani yake.

Hata hivyo Mollel amebainika kuwa  kinara mwenye mradi wa kuwaunganishia maji watu mbalimbali kinyemela, huku wakimlipa kiasi kikubwa cha fedha ,ambapo mamlaka hiyo imengóa mtandao wa mabomba yote aliyoyaunganisha kwa wakazi mbalimbali eneo la Sekei na kufanya familia zaidi ya 20, kukumbwa na adha ya kukosa maji.

Pia meneja  wa maji wa halmashauri ya Arusha, Criston Kimaro ambaye ndiye anadaiwa kutoa idhini ya watu kuunganishiwa maji bila kufuata utaratibu huku watu hao wakimlipa fedha ya kuwaunganishia pamoja na malipo ya mwezi katika kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja.

Operesheni hiyo ikiongozwa na mkurugenzi wa maji safi na maji taka wa jiji la Arusha ,Engineer  Koya na kuambatana na maafisa wengine ,imekuja kufuatia kuwepo taarifa za upotevu mkubwa  wa maji, tofauti na kiwango kinachozalishwa kwa siku na kufanya idadi kubwa ya wateja wake, kutopata huduma ya maji safi baada ya nusu ya maji yanayozalishwa, kuishia njiani kwa wajanja wachache.

Eng,Koya alisema  maji yanayozalishwa na AUWSA ni mengi kutoka katika vyanzo vyake mbalimbali, lakini amekuwa akishangazwa kupata malalamiko ya kila mara kutoka kwa wateja wake wa kudumu na wapya kwamba hawapati huduma hiyo.

Alisema Operesheni hiyo ni yakudumu lengo ni kuhakikisha wanaondoa mtandao wa wezi wa maji, ambao wamekuwa wakijinufaisha bila kuilipa chochote mamlaka hiyo,na kwamba  watawafikisha mahakamani watu wote waliohusika na wizi huo wa maji iwapo watashindwa kulipa fidia katika kiwango walichotumia .

Naye mkuu wa kikosi cha operesheni wa AUWSA,Mohamed Isumail alisema, tangu kuanza kwa zoezi hilo,Mei 29 mwaka huu watu zaidi ya 100 kutoka maeneo ya Moshono,Sekei,Lemara  na Ungalimited wamekamatwa, baada ya kubaini  wamejiunganishia  huduma ya maji na kutumia kinyume na utaratibu .

Aidha alisema maeneo yaliyokithiri kwa wizi wa maji jijini hapa ni ,Sekei,Moshono Migungani na Baraa, ambapo idadi kubwa ya wakazi wa maeneo hayo, wanaiba maji baada ya kuunganisha mipira mirefu chini ya Ardhi huku wakiwahadhaa waofisa wa maji waporika, kuwa maji wanayotumia yanatoka kwenye bomba la kijiji ambayo mara nyingi hayalipiwi.

Isumaili ambaye pia ni kaimu Mhandisi,uendeshaji na matengenezo AUWSA,aliongeza kuwa changamoto kubwa wanayoipata katika zoezi hilo, ni pamoja na watu kujifungia ndani na kugoma kutoa ushirikiano wakati wa zoezi hilo.


No comments:

Post a Comment

KARIBU