..

..
.

Sunday 7 October 2012

WALIO TOSWA NA RAIS KIKWETE NDIYO WAUMINI WA KIFO CHA CCM!

MOJAWAPO ya sifa kubwa atakayokumbukwa nayo Rais Jakaya Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ni kutoa kauli tata ambazo hubakia katika mjadala kwa muda mrefu.


Tofauti kidogo na kauli za hawali safari hii kauli yake imeondoka na vigogo wa chama hicho na kuwatupa nje ya kinyang’anyiro cha kuwania nafasi za uongozi wa jumuiya za chama na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC). 

 Habari kutoka ndani ya NEC, ziliwataja walioenguliwa kuwa ni pamoja na Mbunge wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangalla na Mjumbe wa Baraza Kuu la Vijana la CCM Taifa (UVCCM), Hussein Bashe.



Mbali ya hao, hasira za mwenyekiti huyo wa chama tawala zimemwangukia Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja na Mbunge wa Kahama, James Lembeli.

Wengine waliokumbwa na kadhia hiyo ni pamoja na Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina na Mbunge wa Ludewa, Deo Filukunjombe. Wabunge hao ni miongoni mwa waliotia saini kutaka Waziri Mkuu Pinda ang’oke. Duru za siasa zinasema kuwa msimamo wa wabunge hao kuhusu Pinda, ndio ulisababisha wakatwe kuwania NEC.

Athari za saini za kutaka kumng’oa Pinda ambazo zilisababisha Baraza la Mawaziri lipanguliwe na kuundwa upya, zimeonekana pia kumgusa Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono, ambaye ametupwa nje kuwania nafasi ya uenyekiti wa wazazi CCM taifa. 

Hali ya mkosi bado inaendelea kumwandama Mbunge wa zamani wa Nyamagana, Antony Diallo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza aliyekuwa akitetea nafasi yake, Clement Mabina ambao nao majina yao yamengolewa.



Wakati vigogo hao wakiugulia machungu ya kutoswa, Rais Kikwete ametoa kauli nzito ambayo moja kwa moja inaonekana kuwalenga wahanga hao ya kutaka wagombea waliopata kutoa kauli za vitisho dhidi ya chama hicho kufanya kile walichokusudia kukifanya.  

Akizungumza kwa ukali, Kikwete ambaye juzi alitamba akisema CCM haitakufa kama inavyotabiriwa na baadhi ya watu, alihitimisha kauli yake kwa kusema watu wenye kauli za namna hiyo walikuwa hawafai kuendelea kuwa wanachama wa chama hicho.


Alisema hivi sasa wagombea wengi wamekuwa wakijitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya CCM na kung’ang’ania kupata ushindi kiasi cha wengine kufikia hatua ya kutoa kauli za vitisho kwa kusema wasipopata nafasi ‘patachimbika’.

  “Inashangaza kuona kugombea NEC tu watu wanataka kuuana, wanakimbilia nini huko ndani?” alihoji Rais Kikwete.


“Ina maana watu hawa wanaonyesha dhahiri kuwa hawana nia njema na chama, bali wanaingia kwa maslahi yao binafsi, hivyo tuna kila sababu ya kuwakataa ili tujenge timu ya ushindi ambayo ndiyo nia yetu,” aliongeza mwenyekiti huyo.  

Rais Kikwete alisema kama kuna wagombea ambao watajitoa ndani ya CCM na kuhamia chama kingine kutokana na majina yao kutopendekezwa, wajitoe.


“Hatuchagui wagombea wenye ndimi mbili ambao wanasema kama hatutapitishwa tutahamia chama kingine, hao tunawatakia kila la heri waende tu, kwani hawana nia njema na chama hiki,” alisema.

  Mwenyekiti huyo ambaye alikuwa akizungumza kwa ukali, alisema anajua suala la kuwaengua baadhi ya wagombea litazua mjadala, lakini nia ya chama ni njema katika kuleta sura mpya na uhai.


“Kufanya hivyo ni pamoja na kupata viongozi watakaokiletea chama ushindi katika chaguzi za Serikali za Mitaa 2014 pamoja na Uchaguzi Mkuu mwaka 2015, hivyo lazima watu hao watambue kuwa kazi wanayoifanya ni kuunda timu ya ushindi wa chama na si wa watu.  “Najua kuna ndugu na marafiki ambao hawatateuliwa kutokana na kujaa kwa nafasi na mapungufu na madhaifu ambayo yalionekana baada ya Kamati ya Maadili kupitia majina yao, hivyo wasione kama wameonewa bali wajue kama ndio utaratibu wa chama wa kuhitaji viongozi shupavu, hodari na mwenye uwezo wa kukitetea na kukipigania chama na kukipa ushindi,” alisema Rais Kikwete.

No comments:

Post a Comment

KARIBU