..

..
.

Friday 7 September 2012

TENDWA ANAIDHALILISHA OFISI YA MSAJILI ...


 TUMEZOEA kumsikia Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa akitoa kauli zenye utata na za kukanganya. Kauli zake mara nyingi huwa kali na hulenga kujenga hofu kwa viongozi wa vyama vya upinzani. Kama tulivyosema hapo juu, kauli zake zimezoeleka kiasi cha walengwa kuzibeza, kuzipuuza na kuziita za kutishia nyau.
Ni kauli ambazo mara nyingi hutolewa kwa kukurupuka na pengine ndiyo maana huwa hazifuatiliwi, kwa maana ya kutekelezwa.
 Ni mara ngapi ametoa vitisho vya kufuta usajili wa baadhi ya vyama kwa sababu ya kutoonyesha uhai na kushindwa kufanya kazi za kisiasa kama mikutano ya hadhara, kufungua matawi, kushiriki katika chaguzi, kutafuta wanachama, kufanya maandamano, makongamano na kadhalika? Ni mara ngapi ametoa kauli zenye hisia kali dhidi ya vyama visivyokuwa na ofisi au visivyoitisha mikutano ya wanachama au kuendesha chaguzi kwa njia za kidemokrasia, kwa maana ya kuwaweka au kuwaondoa viongozi madarakani kwa mujibu wa katiba za vyama hivyo? 
Kama tulivyosema hapo juu, kauli hizo hubezwa kwa sababu hazifuatiwi na utekelezaji. Ndiyo maana miaka 20 tangu uanzishwe mfumo wa vyama vingi nchini, asilimia kubwa ya vyama vilivyosajiliwa havina ofisi, havifanyi chaguzi za viongozi, kwa maana ya vyama hivyo kuwekwa mifukoni na viongozi kama mali zao binafsi. Vyama hivyo havifanyi kazi za kisiasa,   haviko hai na havina wanachama wa kuitwa wanachama. Ni vyama vilivyoanzishwa kwa mategemeo kwamba Serikali ingetoa ruzuku kwa kila chama kilichosajiliwa kwa muda au chenye usajili wa kudumu.  
Inawezekana kwamba hutoa kauli kwa hisia kali, tena kupitia vyombo vya habari ili kuonyesha na kuuthibitishia umma na mamlaka iliyomteua kwamba anafanya kazi yake vizuri na kwa ufanisi mkubwa. Lakini pia hufanya hivyo pengine kuonyesha umuhimu wa kuwapo kwa ofisi hiyo ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Hicho ni kitu gani kama siyo kuidhalilisha Ofisi ya Msajili?
  
Kwa njia hiyo, amefanikiwa kuzima kelele za watu ambao wamekuwa wakitoa hoja kwamba msajili huyo hafai kwa kuwa amejidhihirisha kwamba ni ‘simba wa karatasi’ na  kwamba ofisi hiyo ifutwe kwa sababu haina manufaa yoyote kwa vyama vya siasa. Yapo madai mengine mengi kuhusu msajili huyo, ikiwa ni pamoja na kusajili vyama mamluki ili kuvidhoofisha vyama makini na kukisaidia chama tawala wakati wa chaguzi mbalimbali.
  
Hata hivyo, pamoja na msajili huyo kuendeleza kauli zake za vitisho, vyama makini vya kambi ya upinzani vimeshtushwa na kuichukulia kwa uzito mkubwa kauli iliyotolewa juzi na Msajili Tendwa. Wakati wananchi bado wanaomboleza kifo cha Mwandishi Daudi Mwangosi aliyeuawa kikatili na polisi mwishoni mwa wiki mkoani Iringa, msajili huyo alitia chumvi kwenye kidonda alipotishia kuvifuta vyama alivyodai vinakaidi amri ya polisi ya kutofanya mikutano na maandamano, akidai kwamba mikutano hiyo inakuwa na matukio ya vurugu na kusababisha vifo.
  
Tendwa ambaye amekuwa akitishia kuvifuta vyama visivyofanya kazi za kisiasa kama kufanya mikutano ya hadhara, juzi aligeuza kibao na kutishia kukifuta Chadema, akidai kushangazwa na operesheni zake mikoani wakati huu ambapo hakuna kampeni za uchaguzi. Tendwa yuleyule aliyetishia vyama vilivyokuwa vinasubiri chaguzi ndipo vifanye kazi za kisiasa ndiye yuleyule anayesema sasa hakuna kufanya kazi za kisiasa kama hakuna shughuli za uchaguzi.
  
Huyo ndiye John Tendwa anayezuia vyama vya upinzani kufanya shughuli za kisiasa kwa kisingizio cha kuwapo Sensa, huku akikaa kimya siyo tu wakati chama tawala kikiendelea na kampeni za uchaguzi katika Jimbo la Bububu, bali pia kikiendelea na mchakato wa uchaguzi wa viongozi wake nchi nzima kwa wagombea wake kuchukua na kurudisha fomu kwa nderemo na bashasha. Huyo ndiye Tendwa aliyesema juzi baada ya mauaji ya Mwandishi Mwangosi kuwa, polisi wanaporusha mabomu hawakusudii kuua watu, isipokuwa hivyo ndivyo vitendea kazi vyao. Huyo ndiye John Tendwa.

No comments:

Post a Comment

KARIBU