..

..
.

Wednesday 18 July 2012

Urais 2015 wazidi kuwatesa wanasiasa




MBIO za kuwania urais wa mwaka 2015 zimezidi kuwatesa wanasiasa, baada ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe kueleza kuwa hajaoteshwa kuwania kiti hicho, huku Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba akionya kuwa makundi tofauti yanayowania nafasi hiyo ndani ya CCM ni hatari.Membe mbali na kusema hajaoteshwa kugombea urais, ameeleza kuwa ana orodha ya watu kumi na moja wanaomhujumu na kuonya kuwa ipo siku atawataja kwa majina hadharani.
Waziri Membe alitoa kauli hiyo juzi usiku katika Kipindi cha Dakika 45, kinachorushwa na Televisheni ya ITV kila Jumatatu.

Membe alihusisha hujuma hizo na mbio za Uchaguzi Mkuu wa 2015, baada ya kuulizwa ikiwa watu hao wanamfuatafuata kutokana na suala la Uchaguzi Mkuu ujao wa urais.

“Wanajua mambo yote haya, wanaogopa nisiwaguse na wangekuwa na uwezo wangeanza kampeni, labda nioteshwe (urais) na ole wao nikioteshwa ndoto hiyo…” alisema. Waziri Membe na kuongeza:
“Mtu aliye mbaya wako anakuwa na macho matatu. Kwa hiyo kutokana na uwezo wa jicho la tatu anaanza kuzuia lile analoliona lisitokee. Mimi nina macho sita. Nitawataja. Hebu wewe fikiria, kila baada ya miezi miwili naletewa mitego, vituko. Lakini nawaambia Watanzania, waache waseme na mimi ipo siku itakuwa zamu yangu nitawaweka wazi ili kila mtu aelewe.”
“Wasije wakadhani wakijificha kwa wahariri, majumbani kwao ambako ndiyo kuna ofisi zao kwenye ma-godown (maghala) yao ndiyo watakwepa, nitawalipua ili wajue. Ukikaa juu ya nyoka, akigeuka atakuuma tu.”
“Ipo siku nitawaanika hao watu na wapo kumi na moja. Kuna waandishi wa habari mle ndani wawili. Nitawatwanga peupe. Ninyi subirini hata ndani ya Bunge, nitazipangua tuhuma hizo moja baada ya nyingine. Nikimaliza bungeni wajiandae, nitawaanika majina yao, picha zao na mambo yote waliyoandika kwenye magazeti kwa kipindi cha miaka miwili ya uongozi wangu kwenye wizara.”

“Nilikwenda Brazil nikazungumza na Waziri wao wa Mambo ya Nje changamoto anazokumbana nazo akasema ni uongo. Nikamwuliza anapambana nazo vipi akanipa dawa ambayo ni kuwaanika. Nawaambia nitawaanika hapatakalika hapa.”

“Unajua nchi hii kisiasa ina watu ambao wana nguvu nje ya mamlaka ambayo wanayatumia kuvuruga. Wanapenda tuwe na watu wanaovurugika, wasingependa kuona watu wametulia. Ikiwa utaamka na kusema leo nitajivua gamba, leo nitafanya hivi utaandamwa.
Wapinzani na wabunge
Akizungumzia siasa za vyama vingi, Membe alivikosoa vyama hivyo akivitaka viwe makini.
“Naona bado hatujakaa sawa kwa siasa za vyama vingi. Ni kweli, tuna vyama vya upinzani lakini inabidi viwe makini. Kitu ambacho wapinzani hawajui ni kwamba nguvu ya wananchi inaweza kubadilika saa 24, nguvu ya wananchi iko kama bahari ina mawimbi ya kupanda na kushuka,” alisema.
Alisema vipo baadhi ya vyama vya upinzani barani Afrika, vilivyoingia madarakani na kuanguka akisema vilishindwa kutambua nguvu ya wananchi.

Aliwataka wabunge wa upinzani kutumia muda wao mwingi kuangalia majimbo yao badala ya kusema tu bungeni. “Wapinzani ‘reference’ yao iko majimboni siyo bungeni. kipimo chako cha kazi ni jimboni, siyo ukasuku wa kuzungumza bungeni na waandishi wa habari. Nendeni jimboni kwake mkaone uchungu alionao. Lakini siyo anatumia asilimia 100 kuisemea dunia na nchi nzima huku amelisahau jimbo lake,” alisema.
Aliwakosoa pia wapinzani kwa kukosoa bajeti halafu baadaye wanawafuata mawaziri kuwaomba fedha zilizotengwa.

No comments:

Post a Comment

KARIBU