..

..
.

Monday 23 July 2012

RIPOTI MAALUMU Mtandao wa wahamiaji haramu nchini wafichuka

BIASHARA haramu ya usafirishaji binadamu hasa raia wa Somalia na Ethiopia kwenda nchini Afrika Kusini kupitia Tanzania, inazidi kushika kasi mkoani Kilimanjaro ikihusisha wafanyabiashara wakubwa  na vigogo wa Serikali.
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi upande wa Kenya katika maeneo ya Kitobo, Taveta, Ilasiti na Loitokitoki, umebaini kuwa zaidi ya Wahabeshi na Wasomali 1,200 wapo mpakani upande wa nchi hiyo wakisubiri kuvuka, kuingia Tanzania.
 Hata hivyo, jitihada za Serikali kudhibiti biashara hiyo zinaonekana kama mchezo wa kuigiza kutokana na ukweli kwamba wahamiaji haramu hao wanapokamatwa, hurudishwa hadi mpakani na kuachwa upande wa Kenya, ambapo mawakala wa wahamiaji hao haramu wakiwamo Watanzania huwakusanya tena na kuandaa upya safari zao.
 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz amekiri kuwa biashara hiyo kuzidi kushamiri akieleza kuwa ni kutokana na baadhi ya wananchi kukosa uzalendo.  Uchunguzi huo uliofanywa wiki iliyopita umewezesha kupatikana kwa taarifa zinazodai kwamba kinara wa biashara hiyo yupo Mombasa, Kenya.
Imedaiwa kuwa kinara huyo huwalipa mawakala kati ya Dola 2,000 na 4,000 za Marekani ambazo ni sawa na kati ya Sh3 milioni na Sh6 milioni kwa kila mhamiaji haramu anayesafirishwa kutoka Mombasa hadi Malawi.
Habari zinaeleza kuwa wahamiaji hao haramu huingia mkoani Kilimanjaro kupitia njia za panya za mipakani zilizopo katika Wilaya za Siha, Rombo, Same, Mwanga, Moshi Vijijini na kuhifadhiwa kwenye nyumba za wenyeji. “Sasa kuhifadhi wahamiaji haramu ni 'deal' (biashara), kwa sababu wenyeji wanalipwa kati ya Sh100,000 hadi Sh500,000 kwa siku kulingana na idadi ya wahamiaji,” alidokeza mkazi mmoja wa Tarakea, Rombo.
Maeneo ambayo yamekithiri kwa kuingiza wahamiaji hao ni Tarakea wilayani Rombo, Kitobo, Kilototoni, Mabungo Moshi Vijijini, Chekereni na Kifaru wilayani Mwanga.
Mbali na jitihada za vyombo vya dola kudhibiti biashara hiyo, wahamiaji hao bado wamekuwa wakiingia mkoani Kilimanjaro, huku wengine wakifichwa katika mapori wilayani Mwanga.
Wahamiaji wanavyoingia Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili umebaini kuwa kwa maeneo ya Moshi Vijijini, wahamiaji hao haramu huanzia eneo la Kitobo na kusafirishwa kwa pikipiki ambazo hulipiwa Sh20,000 kwa kila safari.
Wahamiaji wengine haramu hupelekwa, kuhifadhiwa katika nyumba zilizopo Mabungo, Kifaru na Kilototoni, ambapo huhudumiwa kwa kupewa mikate mikavu, maji ya kunywa ya chupa na chakula kingine.
Wilayani Rombo, wahamiaji haramu hao huingizwa nchini kupitia Vijiji vya Nayeme, Leto na Kikelelwa na kuhifadhiwa kwa muda katika nyumba za wenyeji kabla ya kusafirishwa hadi Chekereni.
“Kutoka hapa Rombo wanasafirishwa kwa magari aina ya Toyota Noah, mengine yanamilikiwa na polisi na pia malori aina ya Fuso… Hii ni deal (biashara) ya watu wazito,” alidokeza mkazi mmoja aliyeomba jina lake lihifadhiwe kwa sababu za kiusalama.
Mbali na wilaya hizo, katika Wilaya ya Mwanga, wahamiaji haramu huhifadhiwa katika Vijiji vya Kivisini, Ziwa Jipe,Toloha na husafirishwa hadi karibu na Hifadhi ya Mkomazi au Ndungu.
Njia mpya
Uchunguzi umebaini pia njia mpya inayotumika kuwaingiza wahamiaji hao, ambayo vyombo vya ulinzi na usalama havijaweza kuibaini ikianzia Mwanga kwenda Nyumba ya Mungu, hadi Orkasment wilayani Simanjiro.

No comments:

Post a Comment

KARIBU