..

..
.

Tuesday 11 December 2012

Katiba mpya haitapatikana kwa fujo, vurugu

Top of Form 

Katika Shehiya ya Magomeni, mkutano ulivunjika baada ya makundi mawili hasimu kuvurugana. Kundi moja linalosadikiwa kuungwa mkono na CCM linataka mfumo wa Muungano uliopo uendelee, yaani Muungano wenye Serikali mbili, wakati kundi la pili linalosadikiwa kuungwa mkono na CUF linataka Muungano wa mkataba na serikali tatu.
MIKUTANO ya kukusanya maoni kwa ajili ya kupata Katiba Mpya imeingia dosari kisiwani Unguja baada ya baadhi ya wanasiasa na wafuasi wao kuvamia mikutano hiyo na kusababisha ghasia, huku baadhi ya watu wakijeruhiwa kwa kuchomwa visu.
Vurugu hizo zilitokea mwanzoni mwa wiki katika shehiya za Mpendazoe na Magomeni katika Mkoa wa Mjini Magharibi na kusababisha kuahirishwa kwa mikutano hiyo kwa kuhofia usalama wa wananchi. Tukio la baadhi ya watu kuchomwa visu katika Shehiya ya Mpendazoe lilitokana na baadhi ya vijana kuvamia mkutano huo na kufanya fujo.

Katika Shehiya ya Magomeni, mkutano ulivunjika baada ya makundi mawili hasimu kuvurugana. Kundi moja linalosadikiwa kuungwa mkono na CCM linataka mfumo wa Muungano uliopo uendelee, yaani Muungano wenye Serikali mbili, wakati kundi la pili linalosadikiwa kuungwa mkono na CUF linataka Muungano wa mkataba na serikali tatu.
Kutokana na Tume pengine kushindwa kutoa elimu ya kutosha kuhusu mchakato huo, wananchi wengi visiwani humo wamekuwa na dhana potofu kuwa, kundi litakaloonekana kutoa maoni mengi mbele ya Tume kuliko lingine ndilo litakuwa limeshinda, hivyo Katiba itakayotungwa itazingatia zaidi maoni yaliyotolewa na kundi hilo. 
Vurugu zinazotokea katika mikutano mingi ya tume hiyo kwa kiasi kikubwa zinachangiwa na hali hiyo ambayo imesababisha wanasiasa kuwasafirisha wafuasi wao kutoka mbali na kuwaleta katika sehemu nyingine ambako mikutano hiyo inafanyikia. Vurugu hizo pia zinasababishwa na wale wanaosafirishwa kutoka sehemu za mbali kulazimisha kukaa mbele ya wenyeji waliowatangulia ili waweze kutoa maoni kwa sababu Tume haina muda wa kutosha kusikiliza maoni ya wananchi wote wanaotaka kutoa maoni yao.
Itakumbukwa kwamba Tume iliweza kugundua mbinu zinazofanywa na baadhi ya viongozi wa makundi mbalimbali ya kijamii nchini, hasa Unguja na Pemba ambapo wanawapa kwa maandishi wanachama na wafuasi wao maoni ya kusoma mbele ya Tume.
Tunaambiwa mbinu hizo hivi sasa zimepamba moto, hasa baada ya kujikita kwa dhana kwamba wingi wa maoni yatakayotolewa kwa Tume kuhusu jambo fulani ndiyo yatakayopewa uzito na Tume hiyo katika kuandika rasimu ya Katiba Mpya.
Ni bahati mbaya kwamba Tume haijafanya juhudi za kutosha kuwaelimisha wananchi ili watambue kwamba jukumu lake siyo tu kukusanya maoni ya wananchi, bali pia kuyaratibu, kuyatathmini na kuyaainisha katika muktadha wa Katiba inayofaa kulingana na matakwa ya wengi. Hapa lazima ieleweke kwamba maoni ya wengi kuhusu jambo fulani siyo lazima yapokelewe na Tume kama itaonekana kwamba yanakwenda kinyume na masilahi ya taifa.
Kwa mfano, pamoja na kwamba asilimia 80 ya wananchi waliotoa maoni yao walitaka mfumo wa chama kimoja uendelee, Tume ya Nyalali ilipendekeza serikalini kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi siyo tu kwa ajili ya kwenda na wakati, bali pia kwamba ndiyo ungesaidia kuhakikisha unakuwapo mshikamano na umoja wa kitaifa. 
Inasemekana kwamba baada ya matukio hayo ya shehiya za Magomeni na Mpendazoe, Tume imelazimika kuuangukia uongozi wa Mkoa ili uingilie kati kwa kuhakikisha unakuwapo ulinzi wa kutosha katika mikutano hiyo. Hatua hiyo imetokana na vitendo vya baadhi ya wananchi, wakiwamo baadhi ya wanasiasa, wawakilishi na wabunge kuwashambulia wajumbe wa tume hiyo kwa maneno ya vitisho na vya kuwadhalilisha.

No comments:

Post a Comment

KARIBU